Matthew 8

Isa Amtakasa Mwenye Ukoma

(Marko 1:40-45; Luka 5:12-16)

1Isa aliposhuka kutoka mlimani, makutano makubwa ya watu yakamfuata. 2 aMtu mmoja mwenye ukoma akaja na kupiga magoti mbele yake, akasema, “Bwana, kama ukitaka, unaweza kunitakasa.”

3Isa akanyoosha mkono wake akamgusa yule mtu, akamwambia, “Nataka. Takasika!” Mara yule mtu akatakasika ukoma wake. 4 bKisha Isa akamwambia, “Hakikisha humwambii mtu yeyote. Lakini nenda ukajionyeshe kwa kuhani, na utoe sadaka aliyoamuru Musa, ili kuwa ushuhuda kwao.”

Isa Amponya Mtumishi Wa Jemadari

(Luka 7:1-10)

5 cIsa alipoingia Kapernaumu, jemadari mmoja alimjia, kumwomba msaada, 6 dakisema, “Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani na amepooza, tena ana maumivu makali ya kutisha.”

7Isa akamwambia, “Nitakuja na kumponya.”

8 eLakini yule jemadari akamwambia, “Bwana, mimi sistahili wewe kuingia chini ya dari yangu. Lakini sema neno tu, naye mtumishi wangu atapona. 9Kwa kuwa mimi mwenyewe ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, nikiwa na askari chini yangu. Nikimwambia huyu, ‘Nenda,’ yeye huenda; na mwingine nikimwambia, ‘Njoo,’ yeye huja. Nikimwambia mtumishi wangu, ‘Fanya hivi,’ yeye hufanya.”

10 fIsa aliposikia maneno haya, alishangaa, akawaambia wale waliomfuata, “Amin, nawaambia, hata katika Israeli sijapata kuona yeyote mwenye imani kubwa namna hii. 11 gNinawaambia kwamba wengi watatoka mashariki na magharibi, nao wataketi karamuni pamoja na Ibrahimu, Isaka na Yakobo katika Ufalme wa Mbinguni. 12 hLakini warithi wa Ufalme watatupwa katika giza la nje, ambako kutakuwako kilio na kusaga meno.”

13 iKisha Isa akamwambia yule jemadari, “Nenda na iwe kwako sawasawa na imani yako.” Naye yule mtumishi akapona saa ile ile.

Isa Aponya Wengi

(Marko 1:29-34; Luka 4:38-41)

14 jIsa alipoingia nyumbani kwa Petro, alimkuta mama mkwe wa Petro amelala kitandani, akiwa ana homa. 15 kAkamgusa mkono wake na homa ikamwacha, naye akainuka na kuanza kumhudumia.

16 lJioni ile, wakamletea watu wengi waliopagawa na pepo wachafu, naye akawatoa wale pepo wachafu kwa neno lake, na kuwaponya wagonjwa wote. 17 mHaya yalifanyika ili litimie lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Isaya kwamba: “Mwenyewe alitwaa udhaifu wetu
na alichukua magonjwa yetu.”

Gharama Ya Kumfuata Isa

(Luka 9:57-62)

18 nIsa alipoona makutano mengi wamemzunguka, aliwaamuru wanafunzi wake wavuke mpaka ng’ambo ya ziwa. 19 oKisha mwalimu mmoja wa sheria akamjia Isa na kumwambia, “Mwalimu, nitakufuata kokote uendako.”

20 pNaye Isa akamjibu, “Mbweha wana mapango, nao ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.”

21 qMwanafunzi mwingine akamwambia, “Bwana, niruhusu kwanza nikamzike baba yangu.”

22 rLakini Isa akamwambia, “Nifuate, uwaache wafu wawazike wafu wao.”

Isa Atuliza Dhoruba

(Marko 4:35-41; Luka 8:22-25)

23 sNaye alipoingia kwenye mashua, wanafunzi wake wakamfuata. 24 tGhafula, kukainuka dhoruba kali baharini hata mashua ikaanza kufunikwa na mawimbi, lakini Isa alikuwa amelala usingizi. 25Wanafunzi wake wakamwendea na kumwamsha, wakisema, “Bwana, tuokoe! Tunazama!”

26 uNaye Isa akawaambia, “Kwa nini mnaogopa, enyi wa imani haba?” Kisha akaamka na kukemea dhoruba na mawimbi, nako kukawa shwari kabisa.

27Wale watu wakashangaa, wakisema, “Ni mtu wa namna gani huyu? Hata upepo na mawimbi vinamtii!”

Wawili Wenye Pepo Waponywa

(Marko 5:1-20; Luka 8:26-39)

28 vWalipofika ng’ambo katika nchi ya Wagerasi, watu wawili waliopagawa na pepo wachafu walitoka makaburini nao wakakutana naye. Watu hawa walikuwa wakali mno kiasi kwamba hakuna mtu aliyeweza kupita njia ile. 29 wWakapiga kelele, “Una nini nasi, Mwana wa Mungu? Umekuja hapa kututesa kabla ya wakati ulioamriwa?”

30Mbali kidogo kutoka pale walipokuwa, kulikuwa na kundi kubwa la nguruwe wakilisha. 31Wale pepo wachafu wakamsihi Isa, “Ukitutoa humu, turuhusu twende kwenye lile kundi la nguruwe.”

32Akawaambia, “Nendeni!” Hivyo wakatoka na kuwaingia wale nguruwe, nalo kundi lote likateremka gengeni kwa kasi, likaingia katika ziwa na kufa ndani ya maji. 33Wale watu waliokuwa wakiwachunga hao nguruwe wakakimbia wakaingia mjini, wakaeleza yote kuhusu yale yaliyowatokea wale waliokuwa wamepagawa na pepo wachafu. 34 xKisha watu wote wa mji huo wakatoka kwenda kukutana na Isa. Nao walipomwona wakamsihi aondoke kwenye nchi yao.
Copyright information for SwhKC